Video yako ikipata “mipaka ya uchumaji wa mapato” au “aikoni ya njano,” unaweza kuomba ifanyiwe ukaguzi na binadamu. Unapotuma ombi la ukaguzi, mtaalamu wa sera hukagua video yako na kufanya uamuzi kuhusu uchumaji wa mapato. Makala haya yanafafanua kinachofanyika wakati wa ukaguzi.
Mambo ambayo wakaguzi hutathmini wakati wa ukaguzi
Wataalamu wetu hukagua maudhui yote yanayohusiana na video. Wakaguzi hutazama na kutathmini kwa umakini kila sehemu ya maudhui, ikiwa ni pamoja na:
- Maudhui ya video
- Mada
- Kijipicha
- Maelezo
- Lebo
Jinsi wakaguzi wanavyotathmini maudhui
Wakaguzi wetu hutathmini video na maudhui yanayohusiana kwa ujumla. Ufaafu wa matangazo wa kila video hutegemea muktadha wake.
Wakati wa ukaguzi, wataalamu hutumia mwongozo wa maudhui yanayofaa watangazaji pamoja na kanuni zifuatazo:
- Muktadha
- Lengo
- Toni
- Uhalisia
- Kiwango cha maudhui ya kuogofya
Kanuni muhimu zaidi ni muktadha. Je, madhumuni ya video yako ni yapi — ni kutaarifu na kuelimisha au kuogofya na kuchochea? Kwa mfano, ikiwa ni kutaarifu na kuelimisha, unapaswa kujumuisha muktadha kwenye mada, vijipicha, maelezo na lebo zako. Muktadha huu huwasaidia wakaguzi kufanya uamuzi unaofaa kuhusu uchumaji wa mapato. Bila muktadha, huenda wakaguzi wasiweze kutathmini maudhui yako kwa usahihi.
Kwa mfano, kunaweza kuwa na video yenye maneno ya matusi na ikapata matangazo. Wakati huo huo, video tofauti isiyo na maneno ya matusi lakini ina kiwango kikubwa cha maudhui ya vita huenda isipate matangazo.
Kinachofanyika baada ya ukaguzi
Baada ya ukaguzi kukamilika, utapokea barua pepe iliyo na uamuzi kuhusu uchumaji wa mapato. Uamuzi wa mkaguzi ni wa mwisho na hali ya uchumaji wa mapato kwenye video haitabadilika tena.
Umuhimu wa ukaguzi unaofanywa na binadamu
Mifumo yetu huendeshwa na teknolojia ya mashine kujifunza na mamilioni ya data ya ukaguzi uliofanywa na binadamu kwenye video zilizokatiwa rufaa. Kwa pamoja, husaidia kufunza na kuboresha mfumo ili ufanye maamuzi yanayofaa kuhusu uchumaji wa mapato kwa kila video. Teknolojia hiyo hulinganisha maamuzi yanayotokana na ukaguzi unaofanywa na binadamu na maamuzi ya kiotomatiki na kutumia maelezo haya kuboresha usahihi wa mfumo.